Mungu kwanza

Wednesday 28 August 2019

NGUVU YA UNACHOSTAHILI NI ZAIDI YA UNACHOTAKA TU




Huwezi kujisikia tu kuweka maji kwenye tank la gari inayotumia petrol, yaani huwezi tu ukapenda kuweka chumvi kwenye chai na sukari kwenye mboga. Huwezi tu ukavaa viatu mikononi hata kama unapenda sana iwe hivo, unawezaje kuvaa shati miguuni kama suruali au gauni? Hebu fikiria kuwa umealikwa kwa ajili ya chakula, halafu unaambiwa agiza chakula upendacho halafu wewe unaagiza chakula kwa woga ukiogopa bei halafu mwishoni unaambiwa ulitakiwa kuagiza bila kuwa na wasiwasi wa bei. Au wewe pata picha umekufa na ukafanikiwa kufika mbinguni, unafika tu unaanza kuonyeshwa kila kitu ambacho ulikuwa utakiwa uwe nacho yaani kila ulichostahili kuwa nacho. Ukaonyeshwa mumeo au mkeo, ukaonyeshwa magari ambayo ungekuwa nayo,unaonyeshwa aina ya maisha ambayo ulitakiwa kuyaishi ukiwa duniani, yaani unaonyeshwa kila aina ya mambo uliyokuwa unastahili kuwa nayo. Wapo watakaolia na kuomba kurudhishwa tena duniani ili waje walipize kisasi kwani walinga’ng’ana na mambo waliyopenda na kutamani kuwa nayo kwa gharama ya yale waliokuwa wanastahili.
Ninachosema hapa ni hiki, kuna utofauti mkubwa sana kati ya unachotaka na unachostahili. Utofauti wake upo kwenye mengi lakini ni pamoja na nani anaekupa na kwa nini anakupa maana kila kimoja kati ya hayo vina nguvu kwa namna yake katika maisha ya mtu. Ukiingia kumuomba Mungu unaombaje, kwamba Baba akupe unachotaka tu ama unachostahili, kumbuka mapenzi ya Mungu kwako ni zaidi ya unachotaka au kutamani bali zaidi sana kile unachostahili. Kutokujua unachostahili ni mtego mkubwa sana unaozaliwa na kutokujijua na kujitambua mwenyewe maana huwezi kujua unachostahili kama hujijui. Unaweza usinielewe kama utaamua kufanya hivyo lakini wazo la msingi hapa ni jepesi sana kueleweka. Bwana Yesu alishawahi kusema usitoe chakula cha watoto ukampa mbwa, najua alikuwa ana maana yake kwa mazingira yale lakini nataka tu uone kitu hapo. nataka uone kuwa kipo chakula ambacho watoto wanastahili na mbwa wanastahili, huwezi kumpa makombo mtoto halafu mbwa ukampa chakula freshi, lazima uwe na shida.
Changamoto ya mambo unayotaka ni mengi ikiwemo; Unachotaka kimetokana na maisha ya makuzi, yaani umeona na umesikia nini, ulifanyiwa nini wakati unakua, ulikwenda wapi, ulikula nini au ulikuwa unalishwa nini, pia kila tukio lilitokea katika maisha yako lilichangia sana kukutengenezea aina ya mahitaji ambayo yatakuwa na sauti na nguvu kubwa kwako hivi sasa umekua.  Ndo maana utakuwa watu wanasema kuna vyakula hawezi kula, sio kwamba vyakula hivo ni vibaya, la! Ila ikufuatilia utagundua kuwa lazima kuna muunganiko wa kimaana sawa na mambo yaliyotokea katika maisha yake huko nyuma. Watu wameathiriwa na makuzi yao kwa kiwango ambacho ufahamu wake ndio mpaka wa mahitaji yake. Ngoja nikuelezee kidogo utanielewa hapo chini.

Huwezi kumuomba Mungu akupe kitu usichokijua, kama ambavyo huwezi kuomba kitu na hujawahi kukiona au kukikisia labda ufunuliwe au uigize kwa mtu. Mfano, umeenda mbele ya baba yako wa mbinguni halafu anakwambia sema utakacho nikupe, wewe kwa akili zako na ufahamu wako unamuomba akupe baiskeli, hapo sio kosa lako maana hujawahi kuona kikubwa zaidi ya hicho. Hata kama ni gari au baiskeli bado kuna aina nyingi sana za vitu hivyo na kwa hiyo huwezi kuomba usichokijua au kukifahamu. Ni lazima utaomba sawa na ufahamu wako. Huu ndo msingi wa maombi yetu mengi kwa Mungu, huwa tunaishia kuomba tunayotaka tu na kuishia hapo, au tunayotamani na kuishia hapo na kumbe yapo tunayostahili sema tu vile hatupendi kulipa gharama yake. Nitaelezea zaidi hapa chini.
Jambo lolote unalostahili halitokani na maoni ya mtu au maoni yako, hapana. Weka hilo akilini. Kama ilivyo kwa gari, kwamba inatumia mafuta ya diseli au petrol haitokani na maoni ya mtumiaji au muuzaji bali mtengenezaji. Huwezi ukajipangia na kujibadilishia leo ukaanza kuvuta hewa na naitrojeni na huku aliyekutengeneza ameshakuweka oksijeni. Unachostahili ni mawazo halisi ya mtengenezaji au muumbaji wa kitu au mtu. Kila mtengenezaji au muumbaji, moja kati ya tabia yake ni KUKISTAHILIHILISHA kile anachokitengeneza au ile bidhaa, yaani anakiwekea utaratibu na kanuni na faida ndani ya kanuni ili kukifanya hicho kitu kiwe na maisha yenye maana. Gari linastahili kutembea barabarani, samaki baharini au kwenye maji, hii huwezi kubadilisha hata kama unataka au kupenda kwa namna gani. Weka akilini hii.
Unachosathili unaweza ukakijua toka kwenye akili ya mtengenezaji, wengi hutumia hata vijitabu vya maelekezo kuonyesha namna nzuri ya kutumia bidhaa fulani na usiposoma ujue lazima utakosea tu. Kila kilichotengenezwa kina mwongozo na utaratibu wa matumizi yake, haukitumii tu kwa hisia zao ama tu vile unavyopenda au unavyotaka, ama sivyo kitakulipukia na ukabaki kumlaumu mtengenezaji. Mimi na wewe pia tumeumbwa na mtengenezaji ambae ni Mungu. Mawazo yake Mungu, namna anavyotaka sisi tuishi na kufanikiwa ameviweka katika biblia. Biblia inayafunua mawazo halisi ya Mungu juu yetu na kila kitu kuhusu maisha. Mawazo ya Mungu katika uumbaji wetu ndio mambo tunayotakiwa kuyajua maana ndio tutajua tunayostahili badala ya kukesha na tunayotaka tu.
Mtu yeyote mwenye akili timamu anajua kuwa ukipewa uchague kati ya unachotaka na unachostahili atachagua anachostahili maana hicho ndo ukamilifu wake. Unachostahili kina nguvu kubwa sana maana kimefungwa ndani ya hatma yako. Ukikipata unachostahili katika kila hatua ya maisha yako utaanza kuona utofauti wa kuishi maisha ya kubahatisha. Hebu wewe mwenyewe fikiria, upate kazi unayostahili, sio tu kwenda kusomea kozi kwakuwa utapata mkopo, fikiri upate mke au mume unaestahili badala ya kujaribu jaribu kama nguo za Mtumba grade X, fikiria upate kila unachostahili itakuwaje? Ni kweli kwamba vitu vyote ni halali lakini si vyote vinafaa au vinajenga, na hapo ndo utaelewa vizuri kuwa unachostahili ni sehemu ya maisha yako. Wewe endelea kuingia kwenye maombi na ubabe wako wa kijinga na kumuomba Mungu mambo unayotaka na huku unayo mengi sana unayostahili na yako pembeni. Unaomba mkokoteni na ulistahili kumiliki ndege binafsi (ACHA UJINGA), acha kula makombo na chakula freshi kiko menzani, kwani una haraka ya nini? Yaweke haya akilini mwako maana yatakufaa. Wewe jiulize tu hata sasa, makosa mangapi umefanya kwa kulazimisha mambo unayotaka tu?
Ngoja nikukumbushe, aina ya maombi ya mtu anaejua nini anastahili ni kama yale aliyoomba Bwana Yesu, akasema BABA KIKOMBE HIKI KINIEPUKE LAKINI SI KAMA NITAKAVYO MIMI BALI MAPENZI YAKO YATIMIZWE AU KAMA UTAKAVYO WEWE. Kwenye kila uombalo au ufanyalo jifunze kuacha nafasi ya Mungu na mapenzi yake kutimia ili upate unachostahili hata kama ni kigumu. Huu ndo ukweli kwamba kuomba mapenzi ya Mungu kutimia maishani mwetu ndio kiwango cha juu na cha mwisho cha kupata unachostahili maana         Mungu hawezi kukufanyia hila na huku yeye mwenyewe amesema ANAKUWAZIA MEMA. Ile kujua tu kuwa Mungu anakuwazia mema inatosha kukufanya utulie na uache kuhangaika maana umeshapewa uhakika na aliyekuumba na kukutengeneza kuwa anakuwazia mema na kwa hiyo chochote kitokacho kwake lazima kiwe kizuri na kinachokufaa wewe.
Ukweli ni kwamba kujua unachostahili ni moja kati ya suluhisho ya matatizo mengi sana maana inaleta utulivu wa ndani na uhakika way ale tunayohitaji. Ukijua unachostahili hutakuwa tayari kushusha bei maana unajua thamani yako. Ukijua unachostahili hutahangaika na makombo, uikjua unachostahili hutapoteza muda kutembea kwa miguu na huku magari ya moto yamepaki kwenu. Ukijua unachostahili hutadanganyika na vitu vya dunia hii na huku unajua hazina yako iko wapi. Ukijua unachostahili hutawapa mbwa chakula cha mumeo au mkeo(ACHA UJINGA WEWE). Ukijua unachostahili hutakaa na wapiga majungu na huku kinywa chako kimejaa neema na baraka. Kujua unachostahili ni ishara ya juu kabisa ya kujitambua katika Mungu maana yeye Mungu ndio uhalisia wa sisi ni akina nani.
Haya sasa, anza leo kubadilisha kuomba kwako, ukiomba unayotaka na kutamani malizia na unayostahili na kukazia kwenye hayo maana kila zawadi nzuri hutoka kwa baba wa mianga. Usisahau kusema, MAPENZI YAKO YATIMIZWE KWANGU KAMA YANAVYOTIMIZWA HUKO MBINGUNI, usisahau kusema SI KAMA NITAKAVYO MIMI BALI KAMA UTAKAVYO WEWE. Maombi yaliyojengwa katika ubinafsi wa unachotaka tu yatakuchosha, utajiona umeomba sana kuliko ubora na kiwango cha majibu halafu utaanza kuchukia maombi na kuacha kabisa kuomba. Huna cha kupoteza kama utapoea na kupotelea ndani ya mapenzi ya Mungu. Uwe na siku njema. Jesus Up!
YKM JESUS UP 2019

Share:

0 comments:

Post a Comment

Contact

P.o.Box 1404 Mwanza Tanzania
E-mail : frhebron@yahoo.com , frhebron@hotmail.com
Mobile: +255716 423 428 , +255766 710 028

Website Visitors

Copyright © Hebron Fredrick All Rights Reserved Designed and Developed by Hebron Fredrick+255716 423 428